Header Ads

Lukaku Kutua Old Trafford Baada Ya Man United Kukubali Kulipa Paundi million 75

Mshambuliaji wa Everton Romelu Lukaku
Manchester United wamefikia Makubaliano na klabu ya Everton kulipa £75m kumchukua mshambuliaji Romelu Lukaku.
Raia huyo wa Ubelgiji wa miaka 24 alifunga mabao 26 katika Ligi ya Premia msimu uliopita.
United, wamekuwa wakimtafuta Lukaku kwa kipindi kirefu majira haya ya joto.
Baada ya kumpata mshambuliaji huyo, sasa hawana haja tena ya kumtafuta Alvaro Morata wa Real Madrid.
Mazungumzo kuhusu kuhama kwa Lukaku hayahusiani na mazungumzo kuhusu uwezekano wa mshambuliaji wa United Wayne Rooney kurejea Everton.
Klabu hiyo ya Jose Mourinho ina matumaini kwamba itakamilisha usajili wa Lukaku kwa wakati kumuwezesha kujiunga na kikosi cha timu hiyo kitakachosafiri kucheza mechi za kabla ya msimu nchini Marekani Jumapili.
Mshambuliaji huyo alikuwa miongoni mwa orodha ya wachezaji ambao Mourinho aliwasilisha kwa naibu mwenyekiti wa klabu hiyo Ed Woodward kwamba alitaka kuwanunua kabla ya msimu kumalizika.
Awali, ilidhaniwa Lukaku angerejea katika kalbu yake ya awali Chelsea, ambayo alijiunga nayo kutoka Anderlecht mwaka 2011.
Mshambuliaji huyo aliuziwa Everton kwa £28m na Mourinho mkufunzi huyo kutoka Ureno alipokuwa katika kipindi chake cha ukufunzi Chelsea mwaka 2014.
Lukaku ni mteja wa wakala Mino Raiola, ambaye pia huwasimamia Paul Pogba, Zlatan Ibrahimovic na Henrikh Mkhitaryan - wachezaji watatu walionunuliwa na United majira ya joto msimu uliopita.
Mbelgiji huyo alikataa ofa ya juu sana kutoka Everton Machi na kusema: "Sitaki kusalia katika kiwango sawa. Ninataka kujiboresha na najua ni wapi nahitaji kwenda kutimiza hilo."

No comments

Powered by Blogger.